Home » » KESI YA MCHUNGAJI GWAJIMA KUENDELEA WIKI IJAYO .kisakamili hiki........

KESI YA MCHUNGAJI GWAJIMA KUENDELEA WIKI IJAYO .kisakamili hiki........


 
 
Mahojiano baina ya Jeshi la Polisi na Askofu Mkuu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima yaliyokuwa yanatarajiwa kuendelea jana, ikiwa ni siku mbili baada ya kuachiwa kwa dhamana na jeshi hilo, jana yalikwama kuendelea kutokana na kile kilichoelezwa kutoimarika kwa afya ya askofu huyo, na sasa yatafanyika Alhamisi ijayo.

Gwajima alidaiwa kuzimia wakati akihojiwa na makachero wa Polisi waliokuwa wanamhoji, alipojisalimisha alasiri ya Ijumaa iliyopita baada ya kutakiwa kufanya hivyo, kutokana na kufunguliwa jalada la malalamiko ya kumkashifu Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Mwadhama Kardinali Polycarp Pengo.
 
Kutokana na hali hiyo iliyotokea majira ya saa tatu usiku wakati akiendelea na mahojiano yaliyoanzia alasiri, alikimbizwa Hospitali ya TMJ, Mikocheni akiwa chini ya ulinzi wa Polisi hadi aliporuhusiwa kutoka Jumanne wiki hii na baadaye kuachiwa kwa dhamana.
 
Mwanasheria wa Askofu Gwajima, John Mallya alithibitisha kuahirishwa kwa mahojiano kati ya mteja wake na Polisi, akisema mapema jana asubuhi aliripoti Kikuo Kikuu cha Polisi Dar es Salaam kama alivyotakiwa kuripoti kituoni hapo kwa ajili ya mahojiano.
 
Hata hivyo, alisema hakuweza kuhojiwa kutokana na kile kinachoelezwa kuwa afya ya mteja wake haijaimarika vizuri na hivyo wamepangiwa kurudi tena kituoni hapo Aprili 9 mwaka huu, yaani Alhamisi ijayo kwa ajili ya mahojiano.
 
“Mteja wangu alifika kituoni leo (jana) asubuhi kwa ajili ya mahojiano na pia kuripoti kama ilivyoagizwa siku alipopatiwa dhamana, hata hivyo afya yake bado haijaimarika na hivyo imewalazimu polisi wampatie muda zaidi hadi Aprili 9 atakaporudi tena kwa ajili ya mahojiano,” alisema Mallya.
 
Hata hivyo, Mallya alisema hali ya afya ya Gwajima imeanza kuimarika na kadri siku zinavyozidi kwenda, atakuwa na nguvu na ataendelea na kazi zake kama kawaida.
 
Mtumishi huyo alipatiwa dhamana katika Kituo cha Polisi Oysterbay na kutakiwa kuripoti Kituo Kikuu cha Kati kwa ajili ya mahojiano zaidi na kusubiri uchunguzi wa kesi yake ukamilike.

TOA MAONI YAKO HAPA

 
Support : Copyright © 2011. HABARILINE - All Rights Reserved